Single Event

Serikali ya Marekani yawajengea uwezo Wanawake Wajasiriamali kukua Kiuchumi Nchini Tanzania

Serikali ya Marekani  kupitia Programu yake ya  Academy for Women Entrepreneurs (AWE) kwa kushirikiana na Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) imeendesha mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake wajasiliamali ili kukua kiuchumi kwa kuwawezesha kutengeneza Mpango wa biashara zao, jinsi ya kukuza mitaji na kuwaunganisha kimtandao na wafanyabiashara waliofanikiwa.

Akizungumza wakati wa Mahafali ya mafunzo hayo yaliyofanyika  Jumatatu tarehe 6, Juni, 2022 Chuoni Mipango. Mgeni Rasmi ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Mhe. Jabiri Shekimweri  aliishukuru Serikali ya Marekani kupitia Ubalozi wao nchini Tanzania kwa kuendesha mafunzo hayo muhimu na kuwashauri wanawake hao kuendelea kuchangamkia fursa zinazojitokeza ili kukuza uchumi wa nchi.

Kwa upande wake Balozi wa Marekani nchini Tanzania Mhe. Dkt. Donald Wright aliwapongeza wahitimu hao  kwa kumaliza mafunzo hayo, na kuushukuru Uongozi na Menejimenti ya Chuo cha Mipango  kwa kushirikiana na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania kwa  kuwa mwenyeji wa Mafunzo hayo  yaliyoanza tarehe 4 April, 2022 na kuhitimishwa tarehe 6 Juni, 2022.  Pia, alisema kuwa Ubalozi wa Marekani umeongeza kiasi cha  Dola za Marekani Laki Moja kwaajili ya kuendeleza Programu ya AWE  katika Mikoa mingine minne.

Aidha, Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini Prof. Hozen Mayaya katika hotuba yake alisema  Chuo cha Mipango kupitia Kituo chake cha Ujasiriamali na Ubunifu (MEI) kitaendelea kushirikiana na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania kuhakikisha  mafunzo hayo yanaendelea kutolewa Jijini Dodoma na sehemu mbalimbali nchini.

"Chuo cha Mipango kinayo fahari kubwa kuwa mwenyeji wa mafunzo haya , ambapo  baadhi ya wahadhiri wetu walishiriki kuwezesha Programu hii kwa kuratibu na kubadilishana uzoefu na washiriki, pia mmoja wa wahadhiri wetu ameshiriki mafunzo haya ya AWE. Hivyo, ni matumaini yetu kuwa ujuzi na maarifa aliyoyapata  yatawanufaisha wanafunzi na Wafanyakazi wa Chuo."Alisema Prof. Mayaya.

Jumla ya Wanawake Wajasiriamali 31 kutoka Dodoma walishiriki mafunzo  na walitunukiwa Vyeti kutoka Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania.